Yanga yapata ulaini Tunisia

YANGA imepata mteremko kuelekea mchezo wao wa marudiano wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Etoile ya Tunisia, kwani imepata mbinu zitakazowawezesha kuwashika pabaya wapinzani wao hao.https://hivisasa.co.tz/wp-content/uploads/2015/04/Yanga-vs-Stand-21-April-e1429610098405.jpg


Mchezo huo ni wa raundi ya pili ya michuano hiyo ambapo katika mchezo wa kwanza uliopigwa Jumamosi iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.
Matokeo hayo yanaipa kibarua kigumu Yanga mjini Tunis kwani watalazimika kushinda au kupata sare ya zaidi ya mabao 2-2 ili iweze kusonga mbele na kutinga hatua ya mtoano kuwania tiketi ya makundi.
Kwa kufahamu ugumu wa mchezo wa marudiano, Yanga imepanga kufanya kila mbinu wanazoweza ili kuwajengea mazingira mazuri ya kushinda na kuwatoa Etoile.
Miongoni mwa mbinu hizo ni kuwahi mapema nchini Tunisia ili kuzoea hali ya hewa ya huko ambayo ni ya baridi na kukutana na Watanzania waishio huko ili waweze kuwapa mikakati ambayo wanaweza kuitumia kukwepa hila za wapinzani wao hao na kushinda.
Lakini pia, Yanga imepanga kujenga urafiki na wapinzani wakubwa wa Etoile, Esperance Sportive de Tunis (ES Tunis) ili kuona ni vipi wanaweza kushirikiana nao wawape mbinu za kufanya vema katika mchezo wao huo ujao.
Akizungumza na BINGWA, Katibu Mkuu wa Yanga, Jonas Tiboroha, alisema: “Bado tuna matumaini ya kuwatoa Etoile, tumepanga mikakati ya kutosha kutuwezesha kushinda ugenini, ikiwamo kuwahi kwenda Tunisia ili kuzoea hali ya hewa ya kule, kuwatumia Watanzania waliopo mjini Tunis kufahamu ni vipi tunaweza kuwashinda wapinzani wetu.
“Lakini pia tukiwa huko tutakutana na wapinzani wakubwa wa Etoile kuona ni vipi tunaweza kushirikiana nao watusaidie kutupa mbinu za kuwatoa wapinzani wetu.”
Tiboroha alisema kwa jinsi walivyojipanga, hawadhani kama wanaweza kutolewa kirahisi na Etoile kwani hata Kocha Mkuu wao, Hans van der Pluijm amewahakikishia kutekeleza majukumu yake kuelekea mchezo huo.
ES Tunis ni miongoni mwa timu kongwe Tunisia ikiwa inashika nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi ya nchi hiyo kutokana na kujizolea pointi 49 ndani ya mechi 24, sawa na Club Africain iliyopo nafasi ya pili kwa wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.
Etoile wao ndio vinara wa ligi hiyo wakiwa na pointi 50 baada ya kushuka dimbani mara 24.
Na leo Etoile du Sahel watavaana na ES Tunis katika pambano la kukata na shoka ambapo kila timu itapania kushinda ili ijiweke katika mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa.
Iwapo ES Tunis itashinda, itakuwa imefanikiwa kuongoza ligi hiyo kwa kufikisha pointi 51, lakini kama Etoile wataibuka kidedea, watakuwa wamezidi kujikita kileleni mwa ligi hiyo kwa kuwa na pointi 54.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4