Mabeki Yanga wamchefua Pluijm

KOCHA Mkuu wa Yanga Mholanzi, Hans van Der Pluijm, ameelezea kukerwa na uzembe uliofanywa na mabeki wake wa kuruhusu kufungwa kirahisi, huku akionyesha hali ya ukali kwa kila mchezaji aliyeshindwa kutimiza majukumu yake ipasavyo.http://taarifa.co.tz/wp-content/uploads/2014/12/pluijm.jpg
Pamoja na makosa yaliyojitokeza katika mchezo wa juzi wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga waliibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Stand United.
Akizungumza jijini Dar es Salaam , Pluijm alikiri kuwa kikosi chake kilikuwa na bahati ya ushindi katika mchezo huo licha ya upinzani mkali walioupata kutoka kwa wachezaji wa Stand ambao walicheza kwa kiwango cha juu.
Alisema kiungo Simon Msuva na mshambuliaji Amissi Tambwe walikosa nafasi za wazi, ambazo zingeweza kuongeza idadi ya mabao huku akidai soka ni mchezo wa makosa siku zote hivyo lolote linaweza kutokea.
Pluijm aliendelea kusisitiza kwamba, mawasiliano ni kitu muhimu kwa wachezaji wanapokuwa uwanjani, huku akiwashushia lawama wale walioonekana kufanya uzembe wa wazi na kupelekea kufungwa mabao hayo.
Wakati Pluijm anafanya mabadiliko ya kumtoa kiungo Mbrazil, Andrey Coutinho ambaye alionekana bado hajarejea katika kasi yake na kumuingiza Mliberia, Kpah Sherman, hakusita kumweleza makosa ya wazi aliyokuwa akifanya.
Pia Mholanzi huyo hakufurahishwa na baadhi ya matukio yaliyofanywa na beki Mbuyu Twite, ambaye alimpa maneno ya ukali baada ya pambano hilo kumalizika wakati wachezaji wakielekea kwenye vyumba vya kubadilishia nguo.
Alisema atahakikisha anakutana na wachezaji wake na kuzungumza juu ya umuhimu wa kuwepo na mawasiliano uwanjani, ili kuondoa tatizo sugu linalowasumbua kwa muda mrefu sasa.
Yanga ambao wanahitaji pointi sita kuwa mabingwa msimu huu, wanatarajiwa kushuka dimbani tena kesho kuwakabili maafande wa Ruvu Shooting kabla ya kuwavaa Polisi Morogoro wiki ijayo. 
Kwa ushindi huo, Yanga wameendelea kutesa kileleni mwa Ligi Kuu, wakiwa na pointi 49 ikiwa ni tofauti ya pointi saba dhidi ya Azam FC wanaoshika nafasi ya pili kwa kujikusanyia pointi 42.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4