Okwi: akili kubebwa J’mosi

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Simba, Emmanuel Okwi, amemshukuru mwamuzi wa mchezo wao dhidi ya Mtibwa Sugar uliochezwa Jumamosi iliyopita, Abdallah Kambuzi wa Shinyanga, kwa kuongeza dakika tano baada ya dakika 90 za muda wa kawaida, hivyo kuwawezesha kufunga bao pekee lililoipa timu yake ushindi wa 1-0.Emanuel Okwi
Okwi alifunga bao hilo dakika ya tatu kati ya tano za muda wa nyongeza, wakati timu hizo zikiwa hazijafungana katika mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mganda huyo alifunga bao hilo kwa staili ya aina yake, akipiga shuti kali akiwa umbali wa mita 25 kutoka lango la Mtibwa baada ya kupokea pasi kutoka kwa Abdi Banda.
Kabla ya kufunga bao hilo wakati baadhi ya mashabiki wakiwa wametoka uwanjani wakijua matokeo ni suluhu, aliwahadaa mabeki na kumchungulia kipa wa wapinzani wao hao alivyokaa na kupiga mpira mrefu uliokwenda moja kwa moja wavuni.
Okwi alisema miongoni mwa watu anaowashukuru kwa kumpa nguvu ya kutafuta bao ni mwamuzi huyo, baada ya kuongeza dakika hizo tano.
Alisema anaamini kama mwamuzi asingeongeza muda huo, wangeweza kutoka suluhu na Mtibwa kwa kuwa mchezo ulionekana kuwa mgumu kwa pande zote tangu dakika ya mwanzo.
“Nilishakata tamaa ya kufunga hadi pale mwamuzi wa pembeni alipoonyesha dakika tano za nyongeza ndipo nilipoona naweza kufanya kitu kuleta furaha Msimbazi, nashukuru hilo limewezekana, hii ni ishara tosha kuwa tunaweza kumaliza ligi katika nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa mwakani,” alisema.
Ushindi wa Simba juzi, umeiweza timu hiyo kupanda hadi nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara wakiwa na pointi 29 ndani ya michezo 18, nyuma ya Azam wenye pointi 30, kabla ya mchezo wao wa jana na Yanga waliokuwa kileleni wakiwa na pointi 31.-bingwa

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4