Ngassa alamba dume TP Mazembe

MABAO sita aliyofunga msimu uliopita katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na matatu ya Kombe la Shirikisho msimu huu, yamemsafishia njia Mrisho Ngassa kutua TP Mazembe ya DRC, ikiwa ni kutokana na mpango unaosukwa na Mtanzania Mbwana Samatta, anayeichezea timu hiyo.
Msimu uliopita, Ngassa aliifungia Yanga mabao hayo ndani ya mechi nne za hatua ya awali na ya kwanza na kumfanya kuwa miongoni mwa wafungaji bora wa michuano hiyo.
Kutokana na mafanikio hayo, mawakala wa klabu mbalimbali barani Afrika na kwingineko, walianza kufuatilia nyendo za straika huyo kuona kama ana kiwango cha kumwezesha kuzichezea timu zao.
Na kwa kuwa Samatta naye anatoka Tanzania, waliamua kumtumia kujua ubora wa winga huyo machachari.
Kutokana na hilo, Samatta alimtumia ujumbe Ngassa kumtaka kudhihirisha ubora wake wa kucheka na nyavu msimu huu wakiwa wanashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho, jambo ambalo mkali huyo amelifanya ndani ya mechi tatu za kwanza kwa kufunga mabao matatu.
Ngassa alifunga bao lake la kwanza katika mchezo wa marudiano wa raundi ya awali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya BDF XI nchini Botswana, kabla ya juzi kucheka na nyavu mara mbili walipoivaa FC Platinum ya Zimbabwe kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Katika mchezo huo wa raundi ya kwanza ya michuano hiyo, Yanga walishinda mabao 5-1 na hivyo kujiweka katika mazingira mazuri ya kutinga raundi ya pili kuelekea mchezo wa marudiano unaotarajiwa kupigwa kati ya Aprili 1 na 3, mwaka huu.
Akizungumza na BINGWA kabla ya mchezo wa Yanga wa juzi, Samatta alisema: “Mawakala wa timu mbalimbali watakuwa wakimfuatilia Ngassa kwa karibuni mno, hivyo ni jukumu lake kuhakikisha anazidi kufunga ili kujisafishia njia kwa kufunga mabao mengi katika hatua hizi za awali.”
Na kama alivyokuwa akishauri mkali huyo wa TP Mazembe, Ngassa alifanya kweli kwa kufunga mabao hayo, lakini pia akicheza kwa kiwango cha juu kwa kutengeneza mengine mawili yaliyofungwa na Niyonzima na Tambwe.
Japo Samatta hakuweka wazi, lakini inaonyesha Mtanzania huyo ameanza kumpigia debe Ngassa katika kikosi chao, akiamini wanaweza kutengeneza kombinesheni kali kama wawapo pamoja katika kikosi cha timu ya Taifa, Taifa Stars.
Tayari Ngassa ameonyesha dalili za kutoendelea kuichezea Yanga baada ya kumalizika kwa mkataba wake mwishoni mwa msimu huu na kuna taarifa kuwa klabu kadhaa zimeanza kumwinda, ikiwamo Free State ya Afrika Kusini.
Kwa siku za hivi karibuni, Ngassa amekuwa moto wa kuotea mbali, akichangia kwa kiasi kikubwa ushindi wa timu yake hiyo kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa.-Bingwa

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4