MZEE YUSUPH: Naona fahari kuwa na wake wengi

Unafahamu kama Mzee Yusuph anasikia raha kuwa na wake wengi,
huku akihakikisha anawatimizia wote mahitaji yao? Fuatana nami ufahamu
mengi zaidi kuhusiana na suala la ndoa kwa nguli huyo wa muziki wa
taarabu hasa wenye vionjo vya mahaba.
Swali: Katika maisha yako umeoa mara ngapi?
Mzee Yusuph: Nimeoa mara tano,
nilioa mke wa kwanza tukashindwana nikamuacha, wa pili nikamuacha, wa
tatu pia nilimuacha lakini wa nne na wa tano nipo nao.
Swali: Kuna sababu kubwa ambayo unaamini mwanamke akiifanya, huwezi kuvumilia zaidi ya kumuacha?
Mzee Yusuph: Sina kosa maalumu,
inapotokea mwanamke anakuwa mjuba nafahamu ameshachoka ninamuacha aende
zake, lakini kukwambia kuwa hili ni kosa maalumu mwanamke akifanya
namuacha sina.
Swali: Mke wa kwanza ulioa ukiwa na umri gani?
Mzee Yusuf: Naona una nichimba, sijui mpaka nikaangalie cheti changu cha ndoa ila nilioa Zanzibar.
Swali: Inasemekana kuwa unampenda sana Leyla kuliko mke mdogo Chiku. Je, hilo lina ukweli?
Mzee Yusuph: Halina ukweli wowote
ndiyo maana nipo nao wote. Nakili kuwa kama binadamu huwezi kuwapenda
wote sawa, lakini najitahidi kama tulivyoamrishwa na dini niwatimizie
wote sawa na ndivyo ninavyofanya.
Mashallah! Katika kuwajali sawa najisifu mwanaume nimejipanga kuhakikisha hakuna anayenung’unika.
Sababu ya watu kusema nampenda sana Leyla kuliko
bi mdogo ni kutokana na kuwa naye muda mwingi kwa sababu tunafanya kazi
pamoja na kazi yetu inatukutanisha na watu wengi ambao hawauoni upande
wa pili.
Ninapotoka na Chiku hawatajua kwa sababu
hawatakuwa pamoja nasi. Na zipo safari nyingine nje ya kazi natoka na
Leyla na hakuna anayefahamu pale wanapotuona mara nyingi tunakuwa kazini
siyo matembezini.
Swali: Kuna tofauti gani ya kuwa na mke mmoja au wengi?
Mzee Yusuph: Tofauti ipo
kulingana na malengo ya muoaji, kuna wanaooa kwa mapenzi, kupata watoto
wengi pia wapo wanaooa kwa ajili ya kukuza uchumi.
Hayo yote yameainishwa hata katika dini yetu ya
Kiislamu, unaweza kumuoa mtu kwa ajili ya kumstiri labda alikuwa hapati
mume. Vile vile unaweza kumuoa kwa kukuza kipato kwa sababu anaweza kuwa
mchakarikaji mambo yakawa sawa nyumbani.
Lakini kwangu mimi ni mapenzi tu hakuna kingine,
nimewaoa wake zangu kwa sababu nawapenda hayo mengine ni majaaliwa
yanayokuja baada ya kuwaoa kwanza.
Wanaodhani kuoa wake wengi ni kwa ajili ya shughuli ya faragha pekee siyo kweli kuna vitu vingi vinatazamwa.
Asikuambie mtu kuwa na wake wengi kuna raha yake,
unajidai, unajinasibu ukiwa nao wamekuzunguka, huku ukisikiliza manukato
tofauti kutoka kwao na kila mmoja akikudekea anavyotaka na ukimudu
kuwahudumia ndiyo raha zaidi, kama ambavyo mimi nafanya.
Swali: Kuna tabia ya wake wenza kutopatana, unakabiliana vipi na tatizo hilo?
Mzee Yusuph: Siyo tatizo ndiyo
raha ya ndoa ya wake wawili, maana ukisema tatizo kwani lazima kuwa nao.
Nakabiliana nalo kwa kuwa wote wangu najua jinsi ya kuwatuliza na
wakanielewa.
Kizuri zaidi ninapokuwa nao hakuna anayeonyesha
kukerwa na mwenzake wote wapo huru kuniambia chochote wanacheka na
kufurahi, kama kuna hali tofauti wanapokuwa wawili hainishughulishi hadi
niwaone ndiyo nitaliita tatizo maana watakuwa wameshanishinda.-mwananchi
Maoni
Chapisha Maoni