Kocha Platinum ajuta kuifahamu Yanga

KOCHA wa Platinum ya Zimbabwe, Norman Mapeza, amesema hatakisahau kikosi cha Yanga kutokana na kuwafanyia mauaji katika mchezo wa kwanza wa raundi ya kwanza ya Kombe la Shirikisho barani Afrika, uliopigwa juzi kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Norman Mapeza
Katika mchezo huo uliokuwa na msisimko wa aina yake, Yanga ilishinda mabao 5-1, wafungaji wakiwa ni Salum Telela, Haruna Niyonzima, Amis Tambwe na Mrisho Ngassa, aliyecheka na nyavu mara mbili.
“Nimekuja Tanzania nikitambua nakuja kucheza na timu imara, nikawasisitiza wachezaji wangu kuwa makini kuepuka kufungwa mabao mengi, lakini wameshindwa na kujikuta tukifungwa mabao mengi.”
Alisema kuwa kikosi kizima cha Yanga kinatisha, hivyo hawezi kumzungumzia mchezaji mmoja mmoja, zaidi ya kuona wanakwenda kujipanga vipi kwao waweze kulipiza kisasi.
Aliionya Yanga kutobweteka na ushindi wao huo na kujiona wamefanikiwa kuwatoa, kwani iwapo wao wameweza kupata mabao matano wakiwa nyumbani kwao, nao hawashindwi kupata idadi kama hiyo wakiwa Zimbabwe.
Wakati huo huo, Haruna Niyonzima amesema siri kubwa ya ushindi mnono walioupata juzi ni mshikamano na umoja walioonyesha wachezaji na viongozi wao.
“Umoja na mshikamano ambao wachezaji na viongozi wameuonyesha ndio umetupa mafanikio haya ya kupata ushindi mkubwa, kikubwa tuendelee kushikamana Wanayanga kazi bado ni ngumu mbeleni,” alisema Niyonzima.-bingwa

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4