Sserunkuma ni habari nyingine

DANNY Sserunkuma ambaye ametua Simba akitokea Gor Mahia ya Kenya, leo atajikuta akishuka kwenye Uwanja wa Mkwakwani, jijini hapa, huku akiwa na usongo zaidi wa kucheka na nyavu kuthibitisha ubora wake mbele ya Mkenya, Rama Salim.

Mganda huyo na Salim walicheza pamoja katika safu ya ushambuliaji ya Gor Mahia kwenye Ligi Kuu ya Kenya, ambapo wawili hao walikuwa ni moto wa kuotea mbali katika kucheka na nyavu.

Kwa kiasi kikubwa, wawili hao ndio waliotoa mchango mkubwa kwa Gor Mahia kutwaa ubingwa wa Kenya mara mbili mfululizo, wakifunga mabao muhimu katika mechi za timu hiyo.http://api.ning.com/files/lQ0QUhfJdPH3clEPGgip55xJJqfb2yRLfvpv1jYYpHG7WGe1NvjVBbexK*lKZRoqwrmLn0XizapiW8qXb-am-abjsWdIBTTE/sserunkuma22.jpg

Lakini baada ya mambo ya kiuchumi kwenda kombo kwenye kikosi hicho cha Kenya, Sserunkuma alijikuta akitua Simba na Salim Coastal Union, japo walikuwa wakipendwa mno na wapenzi wa klabu hiyo.

Sserunkuma, ambaye alianza kuitumikia Simba kwa kusuasua, tayari ameanza cheche zake, akiwa amefunga mabao matatu katika mechi tatu za hivi karibuni za Ligi Kuu Bara.

Hali hiyo inaonekana kuanza kumjenga kisaikolojia kumwezesha kuendeleza makali yake leo dhidi ya Coastal, kama alivyokuwa Gor Mahia ambako aliibuka mfungaji bora wa ligi ya Kenya kwa misimu miwili mfululizo.

Salim alizungumza na BINGWA jana ambapo hakusita kueleza jinsi anavyofahamu uwezo wa kufunga mabao alionao Sserunkuma, hivyo kujipanga kumkabili kwa tahadhari kubwa.

Alisema kuwa Sserunkuma ni mshambuliaji mzuri, lakini pia ni mfungaji bora, hivyo amewatahadharisha mabeki wao kumpa uangalizi wa hali ya juu leo.

“Hapa tulipo hatuweki vichwa chini kutokana na kuuangalia mchezo huo kwa makini mno, tunahitaji kushinda na tumejiandaa kwa hilo, kwani hatuwezi kukubali kupoteza mechi mbili kwenye uwanja wetu wa nyumbani,” alisema.

Coastal Union wanaivaa Simba leo ikiwa ni baada ya kufungwa bao 1-0 na Yanga katika mchezo wa ligi hiyo Jumatano ya wiki hii Uwanja wa Mkwakwani.

Katika msimamo wa ligi hiyo, Simba wapo nafasi ya 8, wakiwa na pointi 16 baada ya kushuka dimbani mara 12, wakati Coastal Union wakishika nafasi ya saba kutokana na mechi 13, wakiwa na pointi 17.-Bingwa


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4