Yanga yafanya usajili wa kutisha

YANGA imefanya bonge la usajili ambao kama utakamilika ndani ya wiki hii, basi kikosi cha timu hiyo kitakuwa moto wa kuotea mbali.
Wanajangwani hao wamemalizana na kiungo mshambuliaji kutoka Brazil, Emerson De Oliveira Neves Roque, baada ya kumpa mkataba wa mwaka mmoja na sasa wanataka kufunga usajili wao kwa kishindo kwa kumleta nchini bonge la straika lenye uwezo wa kutupia mabao kila mara.
Jonas Sakuwaha
Taarifa za uhakika kutoka kwa kigogo mmoja aliyepo kwenye masuala ya usajili zinasema straika huyo atakuwa wa mwisho kusajiliwa katika kipindi hiki cha dirisha dogo la usajili na pia atawasili ndani ya wiki hii kwa ajili ya kumalizana na Wanajangwani hao.
Licha ya kwamba benchi la ufundi la klabu hiyo bado limeficha jina la straika anayekuja, lakini  walikuwa katika mazungumzo ya chini kwa chini na mshambuliaji, Mohamed Traore kutoka Mali ambaye anaichezea El Merreikh ya Sudan.
Mbali na Traore ambaye anasifika kwa upachikaji wa mabao, mabingwa hao wa zamani wa Ligi Kuu Tanzania Bara, walikwenda mbali zaidi na kufanya mazungumzo na Mzambia Jonas Sakuwaha anayeichezea TP Mazembe ambaye naye ni mkali wa mabao.
Kwa sasa baada ya Yanga kumtema Mbrazil Geilson Santos ‘Jaja’ wamebakiwa na washambuliaji wanne tegemeo ambao ni Hamis Kiiza, Jerryson Tegete, Husein Javu, pamoja na Said Bahanuz na wanataka kuleta mtambo mwingine wa mabao.
Kama dili hilo likifanikiwa ni wazi Mganda Hamis Kiiza hatakuwa na chake kwa Wanajangwani hao kwani amekuwa akitajwa mara kwa mara kuondoka kutokana na kiwango chake kutowaridhisha mabosi wake licha ya kwamba hata Niyonzima naye anahusishwa na kutakiwa na Simba na Azam.
Yanga mpaka sasa inao wachezaji watano wa kigeni kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka nchini (TFF), ambao ni Niyonzima, Mbuyu Twite, Andrey Coutinho, Emerson, pamoja na Kiiza ambaye ndiye yupo kwenye mstari mwekundu.
Katika safu hiyo ya ushambuliaji ya Yanga hadi Ligi Kuu inafikia raundi ya saba ni Tegete peke yake ambaye alifanikiwa kupata mabao mawili aliyoyafunga katika mchezo dhidi ya Stand United, huku Javu, Kiiza pamoja na Bahanuzi wakiambulia patupu wakati winga Simon Msuva akiwa kinara kutokana na mabao yake matatu.
Kutokana na ukweli huo ndiyo maana uongozi na benchi la ufundi wakaamua kutafuta straika mmoja mwenye uwezo wa kucheka na nyavu hasa ikizingatiwa kuwa lengo lao kubwa ni kuhakikisha wanarejesha ubingwa wa Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara waliopokwa na Azam msimu uliopita.
Mbali na kujipanga kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu, Wanajangwani hao wanataka kufika mbali katika michuano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika mwakani ambapo wao ndiyo watakaoiwakilisha nchi, huku Azam wakishiriki Ligi ya Mabingwa Barani Afrika baada ya kutwaa ubingwa msimu uliopita.
Msimu uliopita Yanga walikuwa na washambuliaji wakali kama Didier Kavumbagu ambaye alikuwa kinara wa ufungaji kwa upande wa Wanajangwani hao kabla ya kuamua kutimkia Azam ambapo kwa sasa anaongoza akiwa na mabao manne sawa na Dany Mrwanda wa Polisi Morogoro, Ame Ally wa Mtibwa Sugar, pamoja na Rahma Salim wa Coastal Union.
Katika dirisha dogo la msimu uliopita waliamua kuongeza nguvu kwenye safu hiyo ya usajili baada ya kumuongeza Emmanuel Okwi ambaye hata hivyo hakudumu kwa muda mrefu kutokana na kutofautiana na uongozi katika suala zima la malipo na msimu huu kuamua kurejea Simba.-Dimba

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4