Mboob kiboko ya Emerson

KIUNGO mpya wa Simba, Mgambia Omar Mboob, ameanza kwa kukiona cha moto baada ya kuhenyeshwa vilivyo katika mazoezi ya jana, akiandaliwa kumfunika Mbrazil, Emerson de Oliveira Neves Roque wa Yanga, aliyesaini mkataba wa kuichezea timu hiyo jana.
Mboob akiwa na wachezaji wenzake wa Simba, walianza mazoezi ya viungo katika ‘gym’ ya Chang’ombe, Dar es Salaam kabla ya kuhamia ya uwanjani kwenye Uwanja wa TCC Chang’ombe, jijini.
Katika mazoezi hayo ya gym, wachezaji hao walihenyeshwa vilivyo na kujikuta wakiwa hoi na hatimaye kwenda kunyoosha viungo vyao uwanjani kwa kukimbia na kuchezea mpira.
Displaying simba.JPG Mazoezi ya jana hayakutosha kubainisha uwezo wa Mboob kwani yalikuwa ya
kawaida tu.
Usajili wa Mboob umetafsiriwa kama sehemu ya Simba kujibu mapigo ya Yanga waliomsajili kiungo Emerson ambaye vipande vya video vinamwonyesha kama mchezaji aliyekamilika kwa kuwa na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira, kukaba, kupora mipira, kupiga pasi murua, kufunga na mengineyo kama hayo.
Iwapo Mgambia huyo atafuzu, atailazimisha Simba kufyeka mchezaji mmoja wa kimataifa kati ya Amis Tambwe na Pierre Kwizera wote raia wa Burundi.
Mbali ya Kwizera, Simba ina viungo mahiri kama Said Ndemla, Shaaban Kisiga, Wiliam Lucian ‘Gallas’ na Jonas Mkude.
Katika hatua nyingine, Simba imezidi kufanya kweli baada ya kumnasa msaidizi wa Mganda, Joseph Owino katika nafasi ya ulinzi wa kati, ambaye ni beki kisiki wa Mtibwa Sugar, Salim Mbonde.
Tangu kuondoka kwa Mkenya Donald Mosoti ambaye alikuwa akishirikiana vema na Owino, Wekundu wa Msimbazi hao wamekuwa katika wakati mgumu kutokana na safu ya ulinzi wa kati kupwaya.
Isihaka Hassan aliyekuwa akisaidiana na Owino, ameonekana kukosa uzoefu hali iliyotoa mwanya kwa timu pinzani kuipenya safu hiyo.
Simba wamekuwa wakimfukuzia Mbonde kwa muda mrefu kutokana na aina yake ya uchezaji ambapo ameisaidia Mtibwa kuwa kileleni katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, wakiwa na pointi 15.
Taarifa za uhakika kutoka kwa mmoja wa vigogo wa Simba anayeunda Kamati ya Usajili, zinadai kuwa mazungumzo kati ya pande hizo mbili yamefikia mahala pazuri na muda wowote beki huyo atalamba mkataba wa miaka miwili.
“Kwa kweli tumekuwa tukifanya kazi kubwa sana kuhakikisha tunaboresha kikosi chetu, baada ya kufanya hayo kwa Dan Sserunkuma na kufanikiwa kumnasa, hatimaye Mbonde naye ameingia kwenye anga zetu na muda wowote kuanzia sasa tutaingia naye mkataba,” alisema kigogo huyo.
Alisema lengo la kumsajili Mbonde ni kusaidiana na nahodha wao, Owino ambaye amekuwa akifanya kazi kubwa ambapo kwa sasa atapata ahueni kutokana na uwezo wa beki huyo wa Wakata Miwa na kwamba amewataka mashabiki wa Simba kutokuwa na wasiwasi wowote juu ya kikosi chao.
Kabla ya Mbonde kutua Mtibwa, aliwahi kufanya majaribio Simba kuelekea msimu uliopita wakati huo timu ikiwa chini ya Kocha Mkuu, Abdallah Kibadeni na msaidizi wake, Jamhuri Kihwelu ‘Julio’, lakini alionekana si chochote na kuamua kutimkia Manungu, Turiani.
Tangu kutua kwake Mtibwa, amekuwa lulu na sasa Simba wamefanya kila linalowezekana kunasa saini yake.
Msimu huu, Mbone alionekana zaidi katika mtanange wa ufunguzi wa Ligi Kuu Bara wakati Mtibwa walipokutana na Yanga ambapo Wakata Miwa hao waliibuka na ushindi wa mabao 2-0, huku Mbonde akiwazuia vilivyo washambuliaji wa Yanga waliokuwa chini ya Mbrazil, Geilson Santos ‘Jaja’ ambaye amejiengua katika kikosi hicho cha Jangwani.
Mbonde aliendeleza ubabe wake kwa wakongwe wa soka nchini walipomenyana na Simba ambapo aliwadhibiti vilivyo straika wa Wekundu wa Msimbazi hao, wakiongozwa na Mganda, Emmanuel Okwi pamoja na Elias Maguli na mchezo kumalizika kwa sare ya bao 1-1.-Bingwa


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4