Usajili mpya wa Simba


KAMA ulitegemea kwamba Patrick Phiri anapigwa chini pale Simba umekosea. Tulia hapohapo usikie anachosema kiongozi mkuu wa Simba, Rais Evans Aveva.
Amesisitiza kuwa hatamfukuza kocha huyo Mzambia na tayari amempa uhuru wa kuchagua wachezaji anaotaka kuwasajili kwenye dirisha dogo kwa gharama yoyote ile.
Mbali na hilo pia amempa uhuru wa kuchagua wapi timu ikaweke kambi pamoja na mechi za kirafiki anazotaka kucheza wakati huu wa mapumziko ambapo usajili wa dirisha dogo utaanza Novemba 15 hadi Desemba 15.
Aveva ameliambia Mwanaspoti kuwa mashabiki wengi hawakuelewa juu ya taarifa ya kumpa mechi mbili kocha Phiri haikuwa kumfukuza bali ni kuwaandalia taarifa ya kipi ameona ni tatizo na kupelekea timu yao kupata matokeo hayo ya sare mfululizo.
“Hatuwezi kumfukuza kocha kwa matokeo hayo, tulimaanisha kwamba atuandalie ripoti ya kwa nini timu inapata matokeo haya na nini kifanyike, lakini pia tumempa uhuru wa kupendekeza majina ya wachezaji aliowaona kwenye ligi na anataka kuwasajili,” alisema.
“Hiyo iwe kwa wachezaji wa ndani na nje na kwa nafasi anazotaka yeye bila kujali gharama, tumempa uhuru wa kupendekeza timu iweke wapi kambi pamoja na mechi za kirafiki, hivyo mpango wa kumfukuza Phiri haupo.”
Phiri aliwahi kuliambia Mwanaspoti kuwa anahitaji kufanya marekebisho machache katika kikosi chake ambapo alitaja kuwa anahitaji straika, kiungo mkabaji, kipa, mabeki wa pembeni (kulia na kushoto) na beki wa kati.
Kila nafasi anahitaji mchezaji mmoja mmoja.
“Tukimaliza mechi ya Jumapili nitawakabidhi ripoti viongozi wangu ambayo itaambatana na mapendekezo yangu ya usajili, ambapo wao watatakiwa kuyafanyia kazi, sihitaji kusajili wachezaji wengi kwani tutakuwa kama tunaanza upya kujenga timu, nitaangalia nafasi zenye mapungufu,” alisema.
Baadhi ya viongozi wa klabu hiyo wamedai kwamba kocha huyo ni mpole sana kiasi cha kufanya baadhi yao wamwingilie kwenye uamuzi.-Mwanasport

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4