TANZANIA PRISONS YATUA DAR KUIMARISHA KIKOSI CHAKE.



MAAFANDE wa Jeshi la Magereza, Tanzania Prisons, ‘Wajelajela’ wanaendeleza mawindo ya ligi kuu soka Tanzania bara jijini Mbeya na sasa wanajiandaa kucheza mechi mbalimbali za kujipima ubavu.
Kocha mkuu wa Maafande hao, David Mwamwaja amesema vijana wake wanaendelea vizuri na mazoezi, hivyo ana imani kubwa ya kufuta makosa ya msimu uliopita.
“Sisi tupo katika maandalizi mazuri na tunafikiria mambo mazuri katika michezo ijayo,” alisema Mwamwaja. “Tumejiandaa barabara, tumesajili vizuri kwa mujibu wa mapendekezo yangu. Tunajiandaa kuanza na mechi za kirafiki dhidi ya timu ndogo kabla ya kucheza na timu kubwa”
Mwamwaja aliongeza kuwa wataanza na timu za Mbeya ili kuona kama wameimarika na baada ya hapo watasafiri kuja jijini Dar es salaam kwa maandalizi zaidi.
“Tunakuja kucheza mechi za kirafiki Dar es salaam, hapo ni jiji na kuna timu nyingi za kucheza nazo.” Aliongeza Mwamwaja.
Mwamwaja aliichukua Prisons mzunguko wa pili wa ligi kuu msimu uliopita akirithi mikoba ya Jumanne Chale.
Kocha huyo Mkongwe aliweza kuinusuru Prisons kushuka daraja na alisubiri mpaka mechi ya mwisho dhidi ya Ashanti United uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro ili kujua hatima yake.
Katika mechi hiyo iliyokuwa inaamua ni nani kati ya Ashanti na Prisons anabakia ligi kuu, maafande hao walishinda mabao 2 dhidi ya kikosi cha Abdallah Kibadeni.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4