Machumu mshindi tuzo uongozi Afrika Mashariki


Nairobi. Kampuni inayofanya utafiti wa Utawala Bora katika nchi za Afrika ya CEO Titans Building Nations ya Afrika Kusini, imemtunuku tuzo mbili Mhariri Mtendaji Mkuu wa Mwananchi Communications Limited (MCL), Bakari Machumu.
Kampuni ya Mwananchi ndiyo inayochapisha magazeti ya Mwananchi, Mwanaspoti na The Citizens.
Machumu alipata Tuzo ya Uongozi Thabiti katika Vyombo vya Habari vya Tanzania, pia Afrika Mashariki.
Upande mwingine, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi nchini, Titus Kamani naye alikabidhiwa Tuzo ya Utawala Bora katika kipengele cha Watendakazi Bora wa Serikalini wa Afrika.
Machumu na Waziri Kamani walikabidhiwa tuzo hizo juzi usiku katika hafla iliyofanyika Hoteli ya Hilton jijini Nairobi, Kenya.
Kampuni CEO Titans Building Nations inajihusisha na kutambua watu wanaofanya kazi kwa juhudi kwa ajili ya maendeleo ya mataifa yao, hata kuthubutu kuvuka mipaka katika utekelezaji wa majukumu yao.
Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Machumu alisema kuwa amefurahi na ni fahari kubwa kuona kazi yake na taaluma ya habari kwa jumla vikithaminiwa.
“Vyombo vya habari vina jukumu la kuleta mabadiliko katika jamii. Viongozi wa nchi za Afrika wanatakiwa kufahamu mchango wa vyombo vya habari na kushirikiana navyo katika kufikisha habari kwa jamii,” alisema na kuongeza:
“Viongozi wa nchi za Afrika na Tanzania kwa jumla, wanatakiwa kuruhusu watu kuzungumza mambo kwa uwazi na wasifanye vyombo vya habari kuwa ni maadui, bali washirikiane navyo katika kuleta maendeleo.”
Naye Waziri Dk Kamani alisema amefurahia tuzo hiyo na kwamba inaonyesha jinsi wizara yake inavyofanya kazi kwa usahihi na kutambulika hata nje ya mipaka ya Tanzania.
“Nimeshangaa kuona kazi ya wizara yangu imetambuliwa namna hii. Tuzo hii si yangu pekee, bali ni ya wafanyakazi wote wa wizara, pia Watanzania kwa jumla,” alisema.
Waziri huyo alitoa wito kwa viongozi wa Afrika wajitahidi kuwatumikia watu wote ili kusukuma mbele maendeleo.-Chanzo Mwananchi

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4