Serikali kusambaza vipimo vya ebola

 
Serikali imepanga kununua mashine maalumu za kupima joto (thermo-scanners) ili kubaini watu wenye maambukizi ya virusi vya ebola katika viwanja vyote ndege nchini.
Akuzungumzia azma hiyo, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Stephen Kebwe alisema kuwa mashine hizo zitasaidia kubaini maambukizi ya virusi vya ebola kwa haraka katika viwanja vya ndege bila kuathiri safari za abiria.
Dk. Kebwe ambaye alikuwa Afrika Kusini kuhudhuria kikao cha dharula cha nchi wanachama wa Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc), alisema katika kikao hicho walikubaliana kuchukua tahadhari kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo katika maeneo mengine barani Afrika.
Aliongeza kuwa mashine za kupima joto zitasambazwa katika viwanja vya ndege vya Julius Nyerere (JNIA), Kilimanjaro (KIA), Arusha, Zanzibar na Mbeya.
Alisisitiza kuwa bado taifa lina vifaa vya kutosha vya kujikinga na maambukizi ya virusi vya ebola, endapo ugonjwa huo ukifika nchini.
“Niwahakikishie Watanzania kuwa hakuna mtu atakayekufa kwa ugonjwa wa ebola kwa sababu ya kukosa huduma. Hakuna haja ya kuwa na hofu, Serikali tumejipanga kikamilifu kuzuia ugonjwa huu wakati wote,” alisema.
Aprili 2013, Serikali ilipokea msaada wa vifaa maalumu vya kuzuia maambukizi ya virusi vya ebola kutoka Serikali ya Marekani kupitia mpango wake wa USAID. Msaada huo unajumuisha makasha 320 yenye vifaa vya kutosha watumishi wa afya 16,000.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifwani alibainisha  kuwa vifaa vilivyomo katika makasha ni pamoja na magauni maalumu yanayovaliwa na wahudumu wa afya ili kuwakinga kugusana na wagonjwa na vitambaa maalumu wanachovaa  wahudumu juu ya gauni hilo.
Vifaa vingine ni miwani maalumu inayokinga macho, glovu maalumu zinazovaliwa mikononi na kitambaa maalumu chenye dawa ambacho kinatumika kujisafisha endapo mtumishi atapata jeraha lolote wakati  akitoa huduma.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HADITHI:MWALIMU MAGDALENA sehemu ya 1

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 5

Hadithi: Mwalimu Magdalena sehemu ya 4